Uchaguzi mdogo wa ubunge katika majimbo ya Siha mkoani Kilimanjaro na Kinondoni, Dar es Salaam pamoja na kata nne za Tanzania Bara utafanyika Februari 17,2018.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), katika taarifa iliyotolewa leo Januari 3,2018 imesema uchaguzi unafanyika kutokana na waliokuwa wabunge katika majimbo hayo kujivua uanachama na kukosa sifa za kuendelea kuwa wabunge.
Waliokuwa wabunge katika majimbo hayo ni Maulid Mtulia wa Kinondoni kupitia CUF na aliyekuwa Siha, Dk Godwin Mollel walijivua uanachama na kujiunga na CCM.
Taarifa ya Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mkuu mstaafu wa Zanzibar, Hamid Mahmod Hamid imesema kata nne zitakazofanya uchaguzi ni za Isamilo iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza.
Nyingine ni Manzase katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma; Madanga katika Halmashauri ya Wilaya ya Pangani mkoani Tanga; na Kimagai katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma.
Amesema Tume inaendesha uchaguzi baada ya kupokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge, Job Ndugai kuhusu majimbo hayo kuwa wazi.
Jaji Mahmoud amesema barua hiyo ilieleza kuwa majimbo hayo yapo wazi baada Mtulia na Dk Mollel kujiuzulu uanachama wa vyama vyao hivyo kukosa sifa za kuwa wabunge.
Pia, amesema Tume ilipokea taarifa kutoka kwa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa ikiitaarifu uwepo wa nafasi wazi za udiwani katika kata nne za Tanzania Bara.
“Baada ya kupokea barua hizo Tume kwa kuzingatia vifungu vya 37(1) na 46(2) vya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi sura ya 343 pamoja na kifungu cha 13(3) cha Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa sura ya 292 inatangaza kuwa majimbo mawili na kata nne zipo wazi” amesema.
Amesema fomu za uteuzi kwa majimbo hayo mawili na kata nne itakuwa kati ya Januari 14 na 20,2018.
Makamu mwenyekiti huyo wa NEC amesema uteuzi wa wagombea utafanyika Januari 20,2018 na kampeni za uchaguzi mdogo zitafanyika kuanzia Januari 21 hadi Februari 16, 2018 na siku ya uchaguzi itakuwa tarehe Februari 17,2018.
Amevikumbusha vyama vya siasa na wadau wote wa uchaguzi kuzingatia sheria, kanuni, utaratibu, miongozo na maelekezo yote wakati wa uchaguzi huo mdogo.
No comments:
Post a Comment