Thursday, January 4, 2018

Wateja wavurugwa na uamuzi wa BOT



Baada ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kutangaza Benki ya Wakulima Kagera kuwa imefutiwa leseni na kuwekwa chini ya mufilisi baadhi ya wananchi wamefika kwenye benki hiyo ili kujua hatima ya fedha zao na kukuta tayari imefungwa.

Baadhi yao ni wale waliokuwa wamefungua akaunti za vikundi ambao hata hivyo hawakuwahi kuchukua kiasi chao cha fedha baada ya kukuta tayari milango imefungwa na nje kubandikwa taarifa iliyotolewa na BoT kuhusu kufilisika kwa benki hiyo.

Baadhi ya watu hao wamesema walikwenda kupata huduma kama kawaida lakini wakakuta hali hiyo ilivyo.

Mmoja wa wananchi waliokosa huduma Zablon Zakayo amesema waliunda umoja wa mafundi wa uchomeleaji na leo Alhamisi walihitaji kiasi cha 600,000 kwa ajili ya shughuli za mradi wao na kukopeshana.

Amesema kwa hatua huyo ya ghafla mradi wao utayumba na kuomba waruhusiwe kuchukua kiasi cha fedha kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake mwalimu Oscar Anta amesema alifuata kiasi cha fedha kwenye akaunti ya kikundi na kukuta taarifa iliyotolewa na Benki Kuu kuhusu kufilisika kwa benki ya wakulima na kuwa sehemu ya fedha ilikuwa ya wanachama kwa ajili ya ada za shule.

No comments:

Post a Comment